TANZANIA

Makamu wa Rais Tanzania Dk. Mpango Akutana na Naibu Mkurugenzi Mtendaji IMF

JULAI 31, 2023
Border
news image

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango leo tarehe 31 Julai 2023 amekutana na kufanya mazungumzo na Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) Bo Li, Mazungumzo yaliofanyika Ikulu Jijini Dar es salaam.

Katika mazungumzo hayo, Makamu wa Rais amesema Tanzania inathamini ushirikiano uliopo baina yake na Shirika la Fedha la Kimataifa ambao umekua na mchango mkubwa kwa maendeleo ya taifa. Amesema IMF imeendelea kuiunga mkono Tanzania hususani katika kipindi ambacho dunia inapitia changamoto mbalimbali kama vile Uviko19, migogoro ya kimataifa pamoja na mabadiliko ya tabianchi.

Makamu wa Rais ameikaribisha IMF kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kuhakikisha uhimilivu wa kiuchumi na usimamizi wa thamani ya fedha. Amesema serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha uchumi ikiwemo kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji, maboresho ya sera, rasilimali watu, ukusanyaji kodi na utoaji wa elimu ya kodi kidijitali.

Amesema kutokana na mabadiliko ya tabianchi ambayo yameleta athari kwa Tanzania ikiwemo upungufu wa mvua pamoja na mvua zisizotabirika, Tanzania na IMF zinapaswa kushirikiana katika kukabiliana na hali hiyo kupitia mfuko wa mazingira wa IMF.

Kwa upande wake Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) Bo Li, amesema IMF itaendelea kushirikiana na Tanzania kwa kuhakikisha watalaamu wake wanasaidia katika kufanya maboresho ya kiuchumi, kisera na kiutawala. Amesema katika Uhimilivu wa Uchumi, IMF itashirikiana na Tanzania katika kulinda thamani ya fedha hususani katika masoko ya kimataifa pamoja na uwiano wa fedha za kigeni. Pia ameongeza kwamba watashirikiana na Tanzania katika mikakati ya kuongeza ukasanyaji mapato pamoja na kuhakikisha uwiano wa mapato na matumizi unazingatiwa.

Halikadhalika Bo Li amesema IMF itaunga mkono maboresho katika kuimarisha mazingira bora ya biashara, uwekezaji, sekta binafsi pamoja na mapambano dhidi ya rushwa. Amesema mambo hayo ni muhimu katika kupunguza umasikini, kuongeza ajira na kuvutia uwekezaji. Pia ameongeza kwamba shirika hilo litaiunga mkono Tanzania katika kuwekeza kwenye rasilimali watu kama vile sekta za elimu, afya, ulinzi wa jamii ili kuwa na maendeleo jumuishi.

Oliver G Nyeriga - MTV Tanzania