TANZANIA

Shule Salama Mwarobaini wa Ukatili Dhidi ya Watoto - Tanzania

SEPTEMBA 27, 2023
Border
news image

Katika kupambana na matukio ya ukatili kwa watoto mashuleni na majumbani Serikali imeweka mikakati mbalimbali ya kuzuia matendo hayo ikiwemo kutenga sh,trilioni 1.2 kwaaajili ya ujenzi wa shule mpya za sekondari 1,026 nchini Tanzania.

Akizungumza katika kikao kazi cha Maofisa Elimu Mkoa Sekondari na Halmashauri nchini kilichofayika Chuo cha Patandi Wilayani Arumeru Mkoani Arusha,Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais,Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Dk,Charles Msonde aliwataka maofisa elimu hao kuhakikikisha wanasimamia miradi pamoja na kuhakikisha ulinzi na usalama kwa watoto mashuleni umaimarishwa.

Alisema ni lazima sasa walimu waratibu na kusimamia vema usalama na kuzuia ukatili kwa watoto shuleni na katika jamii na kusisitiza mafunzo hayo yataimarisha zaidi uelewa kwa wasimamizi hao ambao muda mwingi hukaa na watoto.

"Lazima mzuie aina zozote za ukatili kwa watoto mashuleni lakini pia kile chakuka cha mchana kinachotolewa mashuleni kinaimarisha afya zao na kuleta usalama zaidi,na msisite kusimamia miradi inayotolewa na serikali kwaajili ya kuimarisha miundombinu mashuleni"

Alisisitiza ujenzi wa shule hizo unaendelea na kuagiza maofisa hao pamoja na walimu kuhakikisha watoto wanaofanyiwa ukatili wanapewa mbinu mbalimbali za kuondokana na mawazo ili waweze kumudu masomo yao darasani

Naye Mratibu Msaidizi wa Mradi wa Shule Salama(SEQUIR) kutoka Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia, Beatrice Mbigili alisema mafunzo hayo ni muhimu kwaajili ya usalama wa watoto mashuleni lakini pia ni vema walimu wakatumia mbinu mbalimbali kuzuia matukio ya ukatili wanaofanyiwa watoto shuleni na nyumbani sanjari na kufuatilia zaidi ili kuchukua hatua.

Wakati huo huo,Mwalimu Ntendeje Kingimali ambaye ni Ofisa Elimu Sekondari Halmshauri ya Wilaya ya Handeni na Mwalimu Benedict Sandi ,Ofisa Elimu Sekondari Halmashauri ya Moshi walisema mafunzo hayo watayasimamia vema ili kuhakikisha matukio ya ukatili wanayofanyiwa wanafunzi yanadhibitiwa ili kuwezesha wanafunzi ambao ni viongozi wa kesho kuwa na ulinzi zaidi na kupata mbinu ya kuyathibiti matukio hayo kwa kuyafichua pale wanapoona wananyanyasika majumbani au shuleni.

Oliver G Nyeriga - MTV Tanzania