TANZANIA

Dkt. Ndumbaro Aiagiza Mikoa Kujiandaa Vyema Mashindano Ya Samia Taifa Cup Tanzania

SEPTEMBA 21, 2023
Border
news image

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo nchini Tanzania Dkt.Damas Ndumbaro ameiagiza Mikoa yote Tanzania Bara na Zanzibar kujiandaa vyema kwa ajili ya mashindano ya Samia Taifa Cup ambayo yatafanyika mwishoni mwa mwaka huu.

Dk.Ndumbaro ametoa maagizo hayo leo Zanzibar wakati akikabidhi vifaa vya michezo kwa wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kwa ajili ya maandalizi ya mashindano hayo ambayo yatahusisha michezo mbalimbali.

"Mwaka huu mashindano yatajumuisha pia Zanzibar na kutakua na Mashindano ya Muziki wa Kizazi Kipya. Lengo la mashindano haya ni kuendelea kuenzi Muungano wetu na kuhakikisha jamii inajishughulisha na michezo, Sanaa na Utamaduni kwakua ni Sekta ambazo zinaibua vipaji na kutoa fursa ya ajira" amesema Mhe. Ndumbaro.

Kwa upande wake Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Mhe.Tabia Maulid Mwita amesema vifaa hivyo vitagawiwa katika mikoa yote ya Zanzibar na mashindano yataanzia katika ngazi ya Shehia mpaka Mkoa ili kupata wawakilishi wazuri Kitaifa.

Miongoni mwa vifaa alivyokabidhi Mhe. Ndumbaro ni pamoja na mipira ya michezo ya mpira wa Miguu, Kikapu na Wavu ambayo kila mchezo mipira 18 huku akiwakaribisha wadau kuiunga mkono jambo hilo katika michezo mingine.

Oliver G Nyeriga - MTV Tanzania